Afisa
Mtendaji Mkuu (CEO) wa Taasisi ya Kusaidia
Mazingira ya Uwekezaji Afrika (Investment
Climate Facility for Africa), Bw. Omar Issa
amekutana na Wajasiriamali wa Kitanzania
waishio Uingereza na kuwapa changamoto ya
kuanzisha biashara nyumbani.
Katika Mkutano
uliofanyika jana katika jengo la Ubalozi wa
Tanzania, London Uingereza (Tanzania House),
Bw. Issa aliainisha fursa nyingi za biashara
zilizopo Tanzania baada ya Serikali kufungua
milango zaidi ya uwekezaji na kupatikana kwa
wawekezaji wakubwa wa Kimataifa.
Akifafanua zaidi mtaalam
huyo alisema hivi sasa takwimu zinaonyesha
kuwa Tanzania inahitaji zaidi biashara za
uwezo wa kati (medium enterprises) ili
kuziba pengo kubwa kati ya wafanyabiashara
wakubwa na wadogo. Alisema ili kuendelea
zaidi kiuchumi, makampuni makubwa yanahitaji
sana makampuni ya kati kwa ajili ya
kutengeneza mali ghafi, kuzalisha nguvu kazi
na kutoa ushauri wa kitaaluma.
Katika Mkutano huo
ulihudhuriwa na watanzania zaidi ya 30, Bw.
Issa aliwashauri wajasiriamali hao kubuni
miradi mbalimbali itakayowawezesha kupata
mikopo kwenye benki za Tanzania ili kuweza
kuanzisha biashara huko nyumbani. Aliwapa
changamoto kuangalia fursa za biashara za
huduma na ushauri wa kitaaluma.
Alisema benki nyingi hivi
sasa nchini Tanzania zinawatafuta wenye
miradi ya uhakika ili kuwakopesha mitaji ya
kufanya biashara nchini humo. Alisema kwa
elimu, upeo na uzoefu waliokuwa nao,
wajasiriamali hao wanaweza kuanzisha miradi
mizuri itakayowezesha kuinua uchumi wa
Tanzania.
Kwa mafanikio zaidi, Bw.
Issa amewashauri wajasiriamali hao kujiunga
katika vikundi ili kuweza kujumuisha utaalam
na mitaji ya msingi ya kuanzisha miradi hiyo.
Alisema biashara nzuri inahitaji utafiti wa
soko, udhibiti na shauku ya maendeleo zaidi.
Katika maswali yao kwa
mtoa mada, wajasiriamali hao walipenda
kufahamu mipango zaidi ya Serikali kuondoa
urasimu. Bw. Issa aliwaambia kwamba wakati
Serikali inaendelea na hatua mbalimbali
kurekebisha mazingira ya uwekezaji na
biashara nchini Tanzania, ni vyema
Watanzania hao pia kutimiza wajibu wao
badala ya kukaa tu kusubiri Serikali kufanya
kila kitu. Alifafanua kwamba Watanzania
walioko nje ya nchi wana uwezo mkubwa sana
wa kubadilisha mazingira ya uwekezaji kama
watarudi nyumbani na kuingiza utamaduni mpya
wa kikazi.
Awali akimkaribisha mtoa
mada, Balozi Mwanaidi Sinare Maajar alisema
kwamba Ubalozi hivi sasa unafanya jitihada
za kuwaunganisha wajasiriamali wa Kitanzania
wa ngazi zote walioko Uingereza ili
kuwashirikisha kikamilifu na Baraza la
Biashara la Tanzania (Tanzania Business
Council).
Bw.
Issa yupo London kwa ajili ya Mkutano wa
Uwekezaji wa Africa (Africa Business Forum
2008) ulioandaliwa na Commonwealth Business
Forum.
Picha zaid za Mkutano huo zinapatikana hapa>>>> |